Monday, September 29, 2008

Muheshimiwa Cobra ndani ya ndege


Honorable Snake inside plane

An Indian flight to Mumbai was grounded at the airport recently after the crew spotted an unexpected guest on board, that is ‘honorable’ Cobra.

Though there have been instances of reptiles moving around the airport, this is for the first time a snake has managed to sneak into an aircraft.

The snake was found inside a domestic aircraft that had arrived from Srinagar. Airline staff on maintenance duty found the snake below a seat.

“There was commotion which scared the snake and it went further inside,: said an airport source. The snake crawled inside a small air vend below the seat after which the staff opened all doors and unscrewed panels.

The airline informed the airport authorities, who called the NGO Wildlife SOS. But the snake remained untraceable. “the plane was fumigated but it seems the snake went further inside the aircraft,” he said.

The snake was found despite repeated checks. “The plane was already late for the Mumbai flight and a spare plane had to be used,” the source said.
-----------

Hindustan Times of Thursday, September 4, 2008

si kila mtumia net ni mpenda ngono


She thinks I watch porn because I surf the net!

heshima kwa watoto ni busara


Baadhi ya kina mama wanapokosa heshima kwa marafiki wa kiume wa mabinti zao...kama huyu mama!

Saturday, September 27, 2008

mambo ya wakubwa

Mmetonaaaaaa wajemeniiii!!!!!!!!




Mama wa shoka Condeleezza Rice akiwa kwenye tizi hakuna mchezooooo!





Hapo safi mama




Zoezi la baiskeli lina raha yake



Kuoga ni muhimu sana



Nadhani hii habari ina ukweli!



Unasema...?



00000000000000000


UN yataka serikali za mitaa ziwezeshwe

Na Maura Mwingira, New York- Marekani

NAIBU Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Dk. Asha-Rose Migiro, amesisitiza wajibu wa serikali za mitaa katika kufanikisha utekelezaji wa malengo ya maendeleo ya milenia (MDG).

Alisema wajibu huo unatokana na ukweli kwamba, chombo hicho ndicho kilicho karibu zaidi na wananchi, ambao ndio walengwa wa MDG.

Dk. Asha- Rose alisema bila ya juhudi za makusudi zitakazozishirikisha serikali za mitaa kuanzia ngazi ya kata, kijiji, wilaya, miji na mikoa, mafaniko yaliyokwisha kupatikana yanaweza kurudi nyuma.

Naibu Katibu Mkuu huyo alikuwa akifungua mjadala kuhusu wajibu na ushiriki wa serikali za mitaa katika utekelezaji wa MDG, ulioandaliwa na serikali ya Italia na kufanyika makoa makuu ya Umoja wa Mataifa.

Mijadala kadhaa ilifanyika jana kuhusu malengo ya milenia, ikifunguliwa na Dk. Asha-Rose; Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika, Rais Jakaya Kikwete na Rais wa Baraza Kuu la 63 la Umoja wa Mataifa, Miguel D’Escoto.

Ahadi ya dola za Marekani bilioni 16 ilitolewa na makundi mbalimbali ya kijamii, zikiwamo taasisi za fedha, wafanyabiashara, nchi wahisani na watu maarufu katika mijadala hiyo.

Dola za Marekani bilioni 1.6 zimetolewa kwa ajili ya usalama wa chakula, dola bilioni 4.5 kwa mpango wa kuendeleza elimu na zingine kwa ajili ya kupamba na malaria.

Kwa mujibu wa Dk. Asha-Rose, ili serikali za mitaa ziweze kutekeleza majukumu yake vizuri, ni muhimu kuwapo kwa utashi wa kisiasa katika kuziwezesha.

“Serikali za mitaa ndizo zinazotoa dira na mwelekeo wa maisha ya wananchi… zinaendesha vituo vya afya na zahanati, shule na kutoa hudumu muhimu kama za majisafi na majitaka.

“Ni lazima tuzisaidie halmashauri hizi ziweze kuzikabili changamoto na kupata nguvu na uwezo wa kutekeleza majumu yake,” alisema.

Dk. Asha-Rose alisema ingawa uwajibikaji wa jumuia za kimataifa ni muhimu katika upatikanaji wa fedha na utaalamu, bado wajibu wa serikali za mitaa katika kufanikisha malengo ya milenia unahitajika.


000000000000000000000000000

Athari za utani wa ‘mchumba’ kwa wasichana

* Mmoja apata mimba na kutelekezwa

NA JANE MIHANJI

JANDO na Unyago ni mila zilizokuwepo zamani ambazo zilikuwa zikiwafundisha vijana maadili mema na jinsi ya kuishi katika jamii.

Kwa mabinti ambao walikuwa wamebalehe hawa waliitwa na mabibi au mashangazi na kupewa mafunzo maridhawa ya maisha kwa jumla. Ikiwa ni pamoja na usafi wa mwili, upendo, uvumilivu, kujituma katika ufanyaji kazi na suala zima la heshima kwa mkubwa na mdogo.

Halikadhalika jando kwa wanaume. Hawa walipelekwa porini kwa makundi yenye umri wa rika moja huko pamoja na kutahiriwa, basi hufundishwa mambo mengi ikiwemo kuwa mioyo ya ujasiri. Tena wakati huo walikuwa wakiingizwa suna bila hata ganzi.

Siku hizi maadili hayo yanapotea, usasa unawaingiza mabinti wa kike kwenye mambo ya ajabu. Vitu kama kitchen party kwa walio wengi ni kufanya mambo ya kishangingi, kuonyesha viungo vyao na michezo ya ajabu.

Kuna baadhi ya watu wamekuwa wakidiriki kuwafundisha mabinti hawa kuwa ni lazima kuwa na mafiga matatu kwani moja haliwezi kuinjika chungu.

Hivi karibuni baadhi ya waandishi wa habari kutoka chama cha Waandishi wa habari za ukimwi na afya (AJAAT) walitembelea wilaya ya Bagamoyo mkoani Pwani na kukutana na baadhi ya mambo ambayo pengine yamesababisha na watoto kutoelezwa bayana madhara ya mambo fulani katika maisha.

Selina (siyo jina halisi) ni binti ambaye alipata mimba bila kujua. Akiwa na bibi yake aliweza kusimulia jinsi alivyopata ujauzito huo aliokuwa hajaupanga.

“Kuna kaka alikuwa akinitania na kuniita mchumba, utani huo uliendelea na alikuwa akinipa vitu vidogo vidogo. Wakati wa sikukuu nilimfuata na kumwomba aniletee zawadi huku nikimwuliza kama kweli atanioa.

“Akaniambia ukitaka nikuoe nipe kidogo nionje.Aliniingiza chumbani kwake na nikafanya naye tendo la ndoa. Alikuwa ni mwanaume wa kwanza na siku hiyo hiyo nilipata mimba,” anasema Selina.

Siku zilivyozidi kwenda alikuwa akijisikia homa za hapa na pale, hadi bibi yake alipokuwa kugundua kwamba ana mimba.

Selina akuwahi kwenda kliniki kuangalia afya yake na hali ile ya ujauzito. Siku moja aliamka asubuhi na kusikia amebanwa na haja. Aliingia chooni na kutaka kumaliza matatizo yake, alipojaribu kujikamua aliona hakuna kitu, aliendelea kukaa chooni na baadaye kusikia kitu kizito kikichoropoka na kusikia mlio.

Kumbe alikuwa amejifungua mtoto wa kiume, alianza kulia na kupiga mayowe, majirani walifika na kumsaidia ambapo mtoto yule aliokolewa. Yaliyomkuta Selina ni kupelekwa katika kituo cha polisi na hatimaye mahakamani kwa kujibu mashitaka ya kutaka kuua.

Wakati huo Selina alikuwa na umri wa chini ya miaka 18. Swali la kujiuliza ni kwamba nani alimfundisha Selina hatari ya tendo la kujamiiana? Nani alipata fursa ya kumweleza dalili za hatari kwa mama mjamzito, au dalili za kutaka kujifungua. Hakuna.

“Jando na Unyago ilijumuisha pia suala zima la mahusiano ya kimwili na elimu ya uzazi pia,” anasema Mustapha Selemani na kubainisha kuwa katika suala zima ya elimu ya afya ya uzazi, wazee walikuwa wakitumia zaidi mbinu za kienyeji kwa maada ya kutumia wakunga wa jadi.

Anasema ilikuwa ni jambo la kawaida wazee kuzalisha mabinti zao nyumbani na hakukua na haja ya watu kwenda hospitali, kwanza kutokana na kuwa mbali na vituo vya afya.

Selina kama mabinti wengine wengi, alikosa elimu ya afya ya uzazi. Magreth Shoo ambaye ni muuguzi anasema kuwa ni vema elimu hiyo ikawa inatolewa shuleni.

“Kuna taasisi mbalimba mbali na vyama vya kijamii siku hizi vimekuwa vikianzisha klabu katika shule mbalimbali za sekondari na kuzungumza na wanafunzi juu ya afya ya uzazi, ukimwi na mambo mengi ambayo chanzo huwa ni mahusiano kati ya wanaume na wanawake,” alisema Magreth.

Hussein Yahya, fundi viatu mtaa wa Lumumba, Dar es Salaam anasema kuwa tabia ya kuzoesha watoto au kuwatania kuita mchumba ni mbaya sana na jamii ikemee.

“Wanaume watu wazima ndiyo wanatabia hii, binafsi siipendi kabisa, mchumba mchumba mwisho inaa mchumba, nimeshashuhudia matukio ya utani wa namna hiyo na baadaye kutokea kwa madhara,” anasema Yahya.

“Akina mama ambao mara nyingi ndiyo huwa na watoto, wakatae tabia hii kabisa siyo nzuri hata kidogo…kwanza mtoto unapomwita hivyo unampa mtihani wa kutaka kujua nini maana ya mchumba, kazi hapo ndiyo inapoanza akija kufahamu, mimi nikisikia mwanangu anaitwa mchumba, huyo mtu tutapambana naye kwasababu nimeshakutana na matukio ya namna hii ambayo baadaye huleta madhara,” aliongeza.

Kwa upande wake, Selina anasema aliona kama ananyanyaswa na kitendo cha kupelekwa polisi na hatimaye mahakamani. Kwani yeye ndiye alikuwa anajua ukweli kwamba hakuwa na nia ya kutaka kumwuua mtoto yule.

“Lakini namshukuru mwanasheria mmoja niliyempata kupita shirika moja la haki za binadamu Dar es Salaam ambaye alinisaidia na nikaachiwa huru. Kwani awali nilikuwa rumande na mtoto. Baadaye nikaachiwa kwa dhamana lakini baadaye kesi haikuendelea,” anasema.

Pamoja na kwamba Selina alibebeshwa mzigo huo mzito na mwanaume, katika tabu zote na misukosuko aliyoipata alijikuta yuko peke yake. Kijana yule alimaliza uhusiano na Selina baada ya kugundua tu kwaba Selina yu mjamzito.

Alimkatisha masomo yake ya elimu ya msingi. Hakuweza kuchukuliwa hatua zozote. Anasema wakati ule hamasa za kuwatia jela wanaopa mimba za wanafunzi hazikuwepo.

Analalamika jinsi maisha yake yalivyokuwa magumu na kusema kuwa asingepata mimba na kuacha shule, pengine angekuwa na maisha mazuri kidogo kuliko ya hivi sasa anayoishi bila kazi.

Selina anasema baada ya kukumbwa na mkasa huo, hapendi kuona mwanamke ananyanyasika au kupata matatizo yanayosababishwa na wanaume.


000000000000000



Watuhumiwa wa ugaidi wabambwa kwenye ndege


* Ni kwa tuhuma za kutaka kufanya ugaidi

COLOGNE, Ujerumani

MAKOMANDO wa Ujerumani wamewakamata watu wawili waliokuwa wanasakwa kwa tuhuma za ugaidi, katika ndege ya KLM iliyokuwa ikijiandaa kuruka kutoka jijini hapa.

Kwa mujibu wa Polisi, watu hao wawili, raia wa Somalia na mwingine msomali aliyezaliwa Ujerumani, inadaiwa walikuwa wakijiandaa kufanya mashambulizi, na wamekamatwa baada ya kufuatiliwa kwa miezi kadhaa.

Ofisa wa Polisi aliieleza televisheni ya hapa, kuwa watu hao walikuwa wakijiandaa kuendesha 'vita vitakatifu', na kwamba taarifa za mipango hiyo zilikutwa nyumbani kwao.

Ndege hiyo ya KLM ilikuwa ikijiandaa kwenda Amsterdam, Uholanzi.

Msemaji wa Jeshi la Polisi,Frank Scheulen, alisema makomando walipanda kwenye ndege hiyo ilipokuwa inakaribia kuruka na kuwakamata watu hao.

Baadaye abiria wote waliamriwa kushuka kwenye ndege hiyo kwa ajili ya kukagua mizigo, kabla ya kuruhusiwa kuruka saa moja baadaye.Ndege hiyo ilitua salama Amsterdam.


00000000000

Kuna mchanga unaohama Ngorongoro


AMA kweli kutembea ni kuona mengi, ndivyo tunavyoweza kusema. Tanzania imejaliwa kuwa na vivutio vya utalii ambavyo wengi wetu hatuvijui.

Katika Hifadhi ya Mamlaka ya Ngorongoro (NCAA) iliyoko mkoani Arusha kuna mchanga unaohama kutoka sehemu moja kwenda nyingine kwa wastani mita 100 kila mwaka.

Mchanga huo umejikusanya mithili ya kichuguu, na ‘husafiri’ kutoka mahali unapokuwa kwenda mashariki mwa hifadhi hiyo.

Kwa sasa, mchanga huo uliopewa jina la kiingereza la ‘moving sand’ uko takribani kilometa 40 kutoka mahali yalipo makumbusho ya Oldupai (Olduvai) ndani ya hifadhi hiyo.

Pamoja na maajabu hayo ambayo yalibainishwa na watafiti wa mambo ya kale waliokuwa wakifuatilia jinsi binadamu wa kale alivyoishi, waligundua pia kwamba huwa hauchani.

Badala yake, husafiri jinsi ulivyo bila kuacha chembe nyuma. Kwa miaka mingi umekuwa kivutio kikubwa cha watalii wanaotembelea eneo la hifadhi.

Watafiti wanasema, aina hiyo ya mchanga hupatikana karibu na ziwa Manyara, lililoko nje kidogo ya hifadhi hiyo.

Wamasai ambao ni miongoni mwa makabila yanayoishi ndani ya hifadhi hiyo huutumia kutoa kafara na kufanya matambiko mbalimbali.

Matambiko hayo hufanywa ili wapate ‘baraka’ kutoka kwa Mungu na pia kuzaa watoto wengi kwa jinsi wanavyopenda. Ili kufanikisha matakwa yao, huchinja wanyama tofauti kama sehemu ya tambiko.


000000000000

Maradhi ya upotevu wa kumbukumbu


BAADHI ya watu wanapofikia umri wa uzeeni hukabiliwa na maradhi ya kupungua uwezo wa kuweka kumbukumbu na hata kuchanganua mambo.

Mazingira ya namna hiyo huweza kuwapata pia baadhi ya watu, bila kujali kuwa wamefikia katika umri huo wa uzee.

Wakati mwingine, mtu mwenye maradhi ya namna hiyo, waweza kudhani ni mwehu, kwa sababu kwa sababu wakati unazungumza naye, anaweza kutamka ghafla jambo ambalo ni kinyume kabisa ama halihusiani na mada mnayozungumzia.

Kwa maneno mengine ya mitaani, vijana husema kuwa mtu wa namna hiyo anapoteza ‘network’.

Haya ni maradhi ambayo yamekuwa yakiwasumbua wengi japokuwa pale yanapotokea kwa wazee, huyachukulia tu ni hali ya uzee.

Wanasayansi wanasema kuwa inapokuwa siyo uzee basi maradhi hayo yanaweza kuoanishwa na ajali ambayo mtu aliipata katika historia ya maisha yake.

Wanasayansi wanasema haya siyo maradhi ambayo mtu anazaliwa nayo bali humtokea akiwa tayari ameanza kuishi.

Kwa kawaida tatizo hilo huanza kwa mtu polepole kupoteza kumbukumbu ikifuatiwa na mtu kushindwa kufanya kazi ambazo kawaida zilikuwa ndani ya uwezo weke.

Hatua inayofuatia anakuwa anachanganya mambo, mathalan ulikuwa umeshinda naye siku nzima anakuuliza, umerudi saa ngapi?
Wewe utashangaa kwanini akuulize hivyo wakati wote mlikuwa pamoja.

Mtu wa namna hiyo pia akienda mahali huweza kusahau njia ya kurudi nyumbani japokuwa inawezekana kabisa alizaliwa na kukulia mazingira yao.

Katika hatua nyingine atapoteza kabisa mawasiliano na hata uwezo wa kujitambua kiasi kwamba hata kama yu uchi hatakuwa na ufahamu wa kujisetiri. Maradhi haya ni tofauti na wehu au utimbio wa ubongo.

Lakini, wanasayansi wanaamini pia kuwa maradhi haya huweza kuwa na uhusiano wa athari za ajali iliyompata mtu muda mrefu ama miaka kadhaa.

Kama kawaida, wanasayansi wapo kwenye tafiti mbalimbali juu ya madhara hayo na hivi karibuni wamekuja na jipya.

Hili ni kundi la wanasayansi wa Chuo Kikuu cha Tiba Washington, Marekani pamoja na Chuo Kikuu cha Tiba Milan, Italia wameweza kutambua jinsi maradhi haya yanavyotokea.

Baada ya pekenyupekenyu zao walibaini kuwa hali hiyo inatokana na mabadiliko ya aina fulani ya protini kwenye ubongo inayojulikana kama amyloid beta.

Wao walibaini kuwa uzalishaji wa aina hii ya protini unapopungua unaongeza uwezekano wa kupatwa na maradhi hayo na inapozaliswa kwa kiwango kinachotakiwa, basi uwezo wa mawasiliano unakuwa katika hali nzuri.

Katika kuendesha utafiti huo, walichukua umajimaji uliopo katikati ya seli za ubongo kwa mtu mgonjwa ambaye alikuwa katika hali mbaya ambayo inahitaji kuwa na usaidizi wa karibu wa madaktari.

Majaribio hayo waliyafanya kwa watu 18 tofauti ambao ndugu zao walitoa ruhusa kwa madaktari hao kufanya hivyo kwa malengo ya utafiti.

Ndipo wakabaini uwepo wa aina hii ya protini lakini, ikabidi wajaribu kuona ni kitu gani kinachochochea kupungua amyloid beta wakati mtu akipata ajali hasa zinazohusiana na maeneo ya kichwa.

Kwa maneno mengine ni kwamba walijaribu kuchunguza kitu kinachosababisha mtu apate ajali, halafu awe amepona kabisa na kuendelea na shughuli zake lakini baadae ghafla maradhi haya yamkumbe.

Profesa David L. Brody wa Chuo Kikuu cha Washington ambaye alikuwa mmoja wa waandamizi kwenye utafiti huo, alisema kuwa kwa kawaida mgonjwa anakuwa tayari na maradhi hayo kabla hajapata ajali.

“Ajali inakuwa tu ni jambo ambalo linaharakisha dalili za ugonjwa huu na siyo kwamba yenyewe ndiyo inasababisha,” alisema Profesa Brody.

Lakini, anasema kuwa bado hawajajiridhisha katika utafiti huu kwa sababu bado kuna mambo ambayo wanapaswa kuyang’amua.

Hii ni pamoja na sababu zinazosababisha ajali kuchochea maradhi hayo na kwa maana kwamba kuathiri uzalishaji wa amyloid beta.

Utafiti wa wanasayansi hao unalenga zaidi katika kuweza kupata dawa muafaka kwa ajili ya kutibu maradhi haya.

Kwa sasa hakina tiba ya moja kwa moja bali madaktari hujaribu kupunguza athari zinazoandamana na maradhi.

Mara nyingi, tiba hii huwa na mafanikio mazuri kwenye hatua za mwanzo za maradhi hivyo tafiti za wanasayansi hawa huenda zikaja na uwezo wa kuzuia na hata kutibu kwa uhakika kwa wale ambao tayari wameathirika.


00000000000000

Utajisikiaje ukigundua gari unalotanua nalo mkeo alihongwa?


WASOMAJI wangu karibuni tena katika safu muipendayo ya Pasua Kichwa, wiki hii nina kitu kingine cha kupasua bongo zenu kisawa sawa.
Kuna jamaa mmoja alikuwa anaishi mitaa ya Ilala, mshikaji tulikuwa tunamuita baharia kwa sababu alifanya sana kazi hiyo zamani katika nchi mbalimbali za Ulaya.
Labda ndugu au jamaa zake wa karibu tu ndio walijua sababu ya kwanini, Baharia alirudi Tanzania na kuendesha maisha kupitia biashara ya nguo na vipodozi.
Jamaa alikuwa na roho nzuri kwa majirani zake na katika kushirikiana kwake na watu mbalimbali, ndipo siku moja akajikuta anamtongoza msichana mmoja wa maeneo ya Kinondoni.
Msichana huyo alikuwa anafanya kazi hoteli moja ya kifahari katika jiji la Dar es Salaam na huenda alikuwa miongoni mwa wakubwa kutokana na gari ya ofisi kumfuata na kumrudisha.
Baharia na msichana huyo wakawa hawakauki machoni mwetu pale mitaa ya Ilala.Wambeya na wakware wa ngono walimmezea mate sana msichana huyo kutokana na kuwa na umbo la kuvutia.
Siwezi kukwambia umbile lake lilivyo ila mitaani baadhi ya vijana hupenda kuwaita wanawake wa kuchora. Yaani paja paja kwelikweli, guu usiseme,kihuno namba nane, shingo kama ya twiga. Nadhani wengi mtakuwa mmeona michoro ya wanawake wa aina hiyo kwenye majarida ya kibongo.
Msichana huyo baada ya kuzama kwenye penzi la Baharia karibu mwaka mmoja, hatimaye wakafunga ndoa.
Kila mmoja alibaki na shughuli zake na mara mwanamke akaanza kubadilisha magari kama njugu. Mara kaja na Toyota Cresta, Sprinter, Suzuki, Prado, Benzi na mengine tele.
Binadamu hakosi wivu. Ghafla Baharia akaanza kuwa mbogo kwa mkewe na hata kufikia kumdunda hadi kumtoa manundu pale alipojibiwa vibaya au kutoridhishwa na majibu ya mkewe.
Jamaa alikuwa anamuuliza mke wake magari hayo ya nani mwanamke anasema yapo aliyonunua kwa fedha zake na aliyopewa na wazazi wake na mengine ya ofisini kwao.
Akiomba nyaraka ili kuthibitisha umiliki hapewi na mwishowe wanaishia kugombana na kupata suluhu wenyewe.
Baharia alikuwa mkali wee mwishowe akalainika kwa kuzingatia alikuwa anaumia roho sana kila alipokuwa anaambiwa atoe talaka kama anaona hayo magari yanamtia wazimu.
Basi akajikuta naye anaendesha moja kati ya magari hayo na siku hiyo Baharia akiwa mitaa ya Magomeni alisimamishwa na jamaa mmoja.
Mwenyewe alijua ni miongoni mwa watu anaojihusisha nao kibiashara,ile kushuka tu kwenye gari akaambiwa kwa sauti kali atoe funguo kabla hajakwenda kulala jela.
Baharia akagoma na kumwambia jamaa ni jambazi, kauli hiyo iliamsha hasira za huyo jamaa na kuanza kumsemea mbovu mwanaume mwenzake.
"Wee nini, hili ni gari langu kama mwanamke wako amekwambia lake kakuficha, leta funguo zangu siwezi kuhonga mwanaume mwenzangu," jamaa alimbwatia Baharia.
Zogo likajaza watu hadi polisi wakafika na kuamua kuwapeleka wahusika kituoni ambako jamaa alikabidhiwa gari lake baada ya kuonyesha nyaraka mbalimbali.
Baharia akawekwa selo ili kutoa maelezo polisi alilipataje, ndugu zake ndio walikwenda kumwekea dhamana akatoka na kurudi nyumbani kwake Ilala kwa daladala, je kama ingekuwa wewe ungefanyaje? tuma katika namba 0777 167514.


00000000

Thursday, September 25, 2008

• Kinyonya kuzikwa Shinyanga kesho

• Kinyonya kuzikwa Shinyanga kesho


Na Mwandishi Wetu

MAZISHI ya mwandishi wa habari wa Kampuni ya Uhuru Publications Ltd (UPL), inayochapisha magazeti ya Uhuru, Mzalendo na Burudani, Ramadhan Kinyonya, yanatarajiwa kufanyika kesho mkoani Shinyanga.
Taarifa iliyotolewa na familia ya marehemu jana ilisema mwili wa marehemu unatarajiwa kusafirishwa kesho asubuhi kwa ndege ya Shirika la Ndege la Precision kwenda Shinyanga na mazishi yamepangwa kufanyika jioni.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, mwili wa marehemu unatarajiwa kuagwa leo saa 7.00 mchana katika Hospitali ya Taifa Muhimbili, Dar es Salaam.
Kinyonya (40), alifariki dunia juzi saa 7.00 mchana katika hospitali ya Muhimbili alikokuwa amelazwa kwa matibabu tangu wiki iliyopita.
Alifikishwa hospitalini hapo kutokana na kusumbuliwa na ugonjwa wa homa ya mapafu.
Kinyonya alijiunga na UPL mwaka jana baada ya kufanyakazi katika magazeti ya Mtanzania, Majira, Mwananchi na Champion.
Hadi mauti yalipomfika, Kinyonya alikuwa mwajiriwa wa UPL, akiwa mwandishi wa habari za michezo wa gazeti la Uhuru.
Kinyonya alizaliwa mwaka 1968 mkoani Shinyanga. Alisoma shule za msingi na sekondari mkoani humo hadi mwaka 1987 alipomaliza kidato cha nne.
Baadaye alijiunga na mafunzo ya upigajipicha, uandishi wa habari na kompyuta ngazi ya cheti.


00000000000

mambo mapya

Mlima Kilimanjaro wazua mzozo mafunzoni Marekani



Na Jacqueline Liana, Milwaukee, Winsconsin

MLIMA Kilimanjaro umesababisha mzozo miongoni mwa Watanzania na Wakenya wanaoshiriki mafunzo ya utawala bora na mapambano dhidi ya rushwa, mjini hapa.

Tukio hilo lilitokea juzi Septemba mwaka huu, wakati wakiwa darasani katika Chuo Kikuu cha Marquette, mjini hapa, chanzo kikiwa ni Dk. Thomas Bausch, raia wa Marekani, aliposema ni katika miaka ya karibuni amefahamu mlima huo uko Tanzania na si Kenya.

“Wamarekani wengi ndivyo wanavyojua, nilishangaa sana,” alisema Dk. Bausch na kuongeza kuwa Watanzania wanatakiwa kuutangaza Mlima Kilimanjaro ujulikane uko kwao.

Kauli hiyo iliwafanya baadhi ya Watanzania wanaohudhuria mafunzo hayo ya wiki sita kujibu kwa msisitizo, kwamba Mlima Kilimanjaro uko Tanzania, huku wakimwambia Dk. Bausch, ‘karibu Tanzania upande Mlima Kilimanjaro’.

Mbunge wa Same Mashariki Anne Kilango Malecela ndiye aliyeongoza ‘mashambulizi’ kwa upande wa Watanzania, kwa kumwambia Dk. Bausch ambaye ni mtu mzima wa makamo kuwa, yeye ni mmoja wa wabunge katika mkoa wa Kilimanjaro na ndiko mlima ulipo.

Baadhi ya Wakenya walikuwa wakiingilia kati wakati Anne alipokuwa akimweleza Dk. Bausch kwa kusema ‘hata ukiwa Kenya unauona Mlima Kilimanjaro.’

Anne aliwataka wanyamaze na kuwaambia kwamba kwa muda mrefu wamekuwa wakieneza uongo huo.

“Huo ni uongo wa kimataifa, Mlima Kilimanjaro uko Tanzania,” alisisitiza Anne na kuongeza “Katika masuala ya msingi yanayohusu nchi yangu sitaki mchezo.”

Anne alitoa mfano kwamba, kama mtu ana nyumba yake, na jirani yake anaiona, je jirani huyo anaweza kutangaza ni yake kwa sababu anaiona akiwa kwake?. Dk. Bausch akajibu hapana.

Mfanyakazi wa Wizara ya Afya ya Kenya, Sylivia Shitsama, alitoa doa zaidi pale alipohoji, kama hiyo nyumba ina manufaa na haitumiwi, kuna ubaya gani kwa mtu mwingine kuitumia. Kauli hiyo ilifuatiwa na mguno wa nguvu kutoka kwa Watanzania, wakiashiria kutokubaliana naye.

Katika hatua nyingine, Dk. Bausch ambaye aliwahi kuwa mshauri wa wanafunzi katika chuo kikuu hicho kwa miaka zaidi ya 10, alisema aliwahi kuzitembelea Tanzania na Kenya. Alisifu Kenya wana chai nzuri, na Anne alimjibu kwamba siku nyingine akirudi Tanzania asikose kuulizia chai ya Njombe kwani nayo ni ‘bomba’.

Watanzania wengine wanaohudhuria mafunzo hayo, ni Naibu Spika Anne Makinda, Mbunge Injinia Mohamed Mnyaa na Ofisa wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Caesar Waitara.

Wengine ni Hakimu Mkazi Batista Mhelela kutoka mkoa wa Ruvuma, Mkurugenzi Mtendaji wa shirika lisilo la kiserikali linalojishughulisha na masuala ya afya mkoani Kilimanjaro, Veronica Shao, Mwenyekiti wa Mahakama ya Ardhi na Nyumba mkoa wa Ilala, Dar es Salaam, Lusungu Hongoli na mfanyakazi wa Bunge, Anselm Mrema.


000

Mlima Kilimanjaro ni salama kupandwa’


‘NA MWANDISHI WETU

SERIKALI imesema mlima Kilimanjaro ni salama kupandwa na si hatari kama ilivyoelezwa na vyombo vya habari vya kimataifa.
Taarifa iliyotolewa jana na Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Blandina Nyoni, ilisema kuwa, hakuna vifo vya watalii wanaokufa ovyo wanapopanda mlima huo.
Ilisema, takwimu sahihi kutoka Shirika la Hifadhi za Taifa (TANAPA) na ofisi ya Kamanda wa Polisi wa mkoa wa Kilimanjaro, zinaonyesha idadi ya wapagazi waliokufa kati ya mwaka 2000 na 2007 ni sita, na kwamba vifo vyao vilikuwa vya kawaida.
“TANAPA inahakikisha kuwa kampuni zote zinazoratibu safari za watalii kupanda mlima Kilimanjaro, zinatimiza vigezo vya usalama kabla ya kuruhusu kundi au mtu mmoja mmoja kupanda mlima huo, “ iliongeza taarifa hiyo.
Mlima Kilimanjaro hupandwa na takribani watalii 40,000 kila mwaka, ambapo mapato yake huingia katika pato la taifa litokanalo na sekta hiyo.
“Taarifa iliyochapishwa siyo sahihi, kilichoelezwa siyo kile kilichotokea katika uendeshaji wa biashara ya utalii katika mlima Kilimanjaro, “ ilisisitiza taarifa hiyo, na kuwataka waandishi waliotoa habari hizo kujitokeza ili kuzirekebisha.
Gazeti la Times Online la Mei 26 na The East African la Juni 2, mwaka huu, yalidai kuwa, wapagazi na waongoza watalii 20 hufariki kila mwaka, na kwamba idadi ya vifo vya watalii ni mara mbili ya hivyo.






Kuondoka Mbeki ni pigo kwa Afrika -JK



Na Maura Mwingira, New York- Marekani

MWENYEKITI wa Umoja wa Afrika (AU), Rais Jakaya Kikwete, amesema kuondoka madarakani kwa aliyekuwa Rais wa Afrika Kusini, Thabo Mbeki, ni tukio la kusikitisha na pigo kwa bara la Afrika.

Rais Kikwete alisema Mbeki ni mmoja wa viongozi wa aina yake, aliyejitolea kusimamia kwa dhati kuhakikisha Afrika inasonga mbele kiuchumi.

Alitoa msimamo huo juzi, alipozungumza na klabu ya waandishi wa habari wa kimataifa, wanaofanya kazi makao makuu ya Umoja wa Mataifa mjini hapa.

Kauli ya Rais Kikwete ilitokana na swali aliloulizwa na mmoja wa waandishi hao, kwenye mkutano uliomhusisha pia Rais wa Benki ya Maendeleo ya Afrika, Donald Kaberuka.

“Niseme tu kwamba hili ni tukio la kusikitisha, ni pigo kwa Afrika. Tumempoteza kiongozi mashuhuri na madhubuti, aliyesimama kidete kuhakikisha Afrika inasonga mbele kiuchumi,” alisema Rais Kikwete.

Mbeki alipangiwa kuwa Mwenyekiti mwenza na Rais wa Bosnia na Herzegovina, Haris Silajdzic, kuendesha mjadala kuhusu changamoto za maendeleo barani Afrika na athari zake katika kufikia malengo ya maendeleo ya milenia.

“Wote tunafahamu na ni mashahidi wa namna Mbeki alivyoasisi na kusimamia utekelezaji wa Mpango wa Ushirikiano Mpya wa Maendeleo Afrika (NEPAD),” alifafanua Rais Kikwete.

Viongozi wakuu wa nchi na serikali wapo mjini New York, kuhudhuria mkutano wa 63 wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa.

Ulitanguliwa na mkutano, ambao viongozi kutoka mataifa ya Afrika, taasisi za fedha na nchi wahisani walijadili namna ya kuogeza kasi ya kusaidia na kusukuma maendeleo ya Afrika.

Rais Kikwete alisema Mbeki pia aliasisi uamsho na uhuishwaji wa ujenzi mpya wa bara la Afrika, uliojielekeza katika ufufuaji wa uchumi, uwezo wa kujenga na kusimamia demokrasia na kutokomeza ukoloni mamboleo kati ya Afrika na mataifa makubwa.

Alisema alikuwa mstari wa mbele na alishiriki kikamilifu katika juhudi za upatanishi na upatikanaji wa amani na demokrasia ya kweli barani Afrika.

Katika hatua nyingine, Rais Kikwete amesema hataraji kwamba, kuyumba kwa soko la hisa na mitaji la Marekani, kunaweza kukawafanya nchi wahisani kushindwa kutekeleza ahadi zao kwa bara la Afrika.

Alisema wakati nchi wahisani na tajiri zilipoahidi kuongeza kiwango cha misaada yao ya maendeleo kwa Afrika, haikuwa imetarajiwa wala kutegemewa kwamba, uchumi wa Marekani ungeyumba.





Soma Majina ya dawa, changamoto zake kwa watumiaji na wasimamizi wa huduma za matibabu

Suala la dawa ni muhimu katika huduma za matibabu. Ipo dhana iliyojengeka miongoni mwa baadhi ya Watanzania kwamba mtu akienda hospitali asipopata dawa au sindano na badala yake akapata ushauri, mtu huyo huwa anajihesabu kama hakutibiwa.

Jina asilia dhidi ya jina la kibiashara (Brand vs Generic) Majina ya dawa na mahali dawa hiyo ilipotengenezwa vimekuwa vikileta changamoto kubwa kwa watumiaji na katika suala zima la tiba hasa kwenye vipengele vya ubora wa dawa husika, uwezo wake wa kutibu na usalama wa dawa hiyo kwa mtumiaji.

Kwa sasa tutaangalia changamoto moja ya majina ya dawa. Hapa ninalenga tofauti iliyopo kati ya jina asilia la dawa (Generic name) na jina la kibiashara la dawa (Brand/Trade name).

Jina asilia la dawa ni nini? Kwanza ningependa kuwafahamisha kwamba kila dawa inayotengenezwa kitaalamu inakuwa na majina matatu kama ifuatavyo: Kwanza jina la kikemikali mfano: Acetaminofen, pili, jina la asilia mfano Paracetamol na tatu, jina la kibiashara mfano Panadol, Sheladol, Tulizamol na mengineyo.

Majina haya yote hapo juu ni majina ya dawa moja paracetamol ambayo wengi wameizoea kwa jina la kibiashara la mtengenezaji mvumbuzi au jina lenye hati miliki (Brand name) yaani Panadol.

Hivyo basi jina asilia la dawa ni lile jina lililokubalika kutumika kimataifa ambapo ukilitaja jina hilo mahali popote duniani mtu anaelewa unazungumzia dawa gani (International Non Propietary Name INN) kwa kufuata mfano wetu hapo juu ni Paracetamol.

Jina la kibiashara la dawa (Brand/Trade name) ni nini? Hili ni jina ambalo kampuni inayotengeneza dawa inaamua kuipa dawa husika. Dawa moja inaweza kuwa inatengenezwa na kampuni nyingi tofauti na kila kampuni ikachagua jina lake ambalo wataona watumiaji watalitambua haraka na kuamua kununua dawa yao badala ya kampuni nyingine.

Mfano Paracetamol inaitwa Calpol, Sheladol, Tulizamol au Cetamol. Hata hivyo, pamoja na dawa kuwa na majina tofauti ya kibiashara kuna jina la kibiashara ambalo dawa hupewa na mtengenezaji wa kwanza wa dawa hiyo mwenyewe.

Mara nyingi dawa hizi za mtengenezaji wa kwanza (mwenye hati miliki) huwa ni ghali sana kwani mtengenezaji anakuwa ametumia muda na fedha nyingi katika utafiti na utengenezaji wa dawa husika, hivyo mtengenezaji huyo hutaka kurudisha gharama alizotumia pamoja na kupata faida wakati watengenezaji wanaofuata hutumia kazi za mtengenezaji wa kwanza kupata faida.

Kwa nini hatimiliki katika dawa? Kwa kawaida dawa huchukua muda wa miaka minane hadi 12 tangu kuvumbuliwa mpaka ianze kuuzwa.Muda huu ni mrefu sana na fedha nyingi huwa zimetumika hivyo mtengenezaji wa dawa kwa mara ya kwanza hupewa muda wa miaka mitano kuuza dawa yake pekee kabla watengenezaji wengine hawajaruhusiwa kuitengeneza ili aweze kurudisha gharama zake.

Na kwa kitaalamu ‘brand medicine’ ni dawa, hizi zinatoka kwa mvumbuzi wa dawa hiyo yaani mmiliki wa hataza (patent owner) na wengine wote wanaofuata kutengeneza dawa hiyo zinaitwa kitaalamu ‘generic medicines’.

Hata hivyo, watu wengi wamekuwa na mazoea ya kuita dawa zote zilizotengenezwa viwanda vilivyoko Ulaya na Marekani ndio ‘Brand Product’ na zile zilizotengenezwa India na nchi za Afrika ndio ‘generic’.

Lakini kitaalamu dawa zinazoitwa ‘brand product’ ni zile zilizotengenezwa na mtengenezaji au mvumbuzi wa dawa wa awali yaani mtengenezaji mwenye hatimiliki.Tofauti kubwa iliyopo kati ya dawa generic na dawa brand kutoka kwa mvumbuzi ni bei kwani dawa ya mvumbuzi huwa ghali sana.

Tofauti nyingine ni katika majina ya kibiashara na viambatanisho vingine vinavyotumika katika kutengeneza dawa husika.Nchi zote zenye mamlaka za kudhibiti dawa haziruhusu utengenezaji au uingizaji wa dawa hizi asilia bila ya kufanyia majaribio ya kutosha kuhakiki kuwa dawa hizi zitakuwa na ubora, uwezo wa kutibu na usalama kwa mtumiaji kama dawa ile iliyotengenezwa na mvumbuzi wa dawa husika (bioequivalence testing).

Hata hivyo kwa nchi zinazoendelea kama Tanzania ambapo asilimia 80 ya dawa zote katika soko zinaagizwa kutoka nje ya nchi, udhibiti wa ubora wa dawa zote katika soko ni mgumu na hivyo kukuta kiasi kikubwa cha dawa bandia (counterfeit) na dawa zisizo na ubora (substandard) ni kubwa katika soko.

Kwa nini orodha ya dawa ya MTBA inatumia majina asilia ya dawa?
Sera ya Taifa ya Dawa inasisitiza uwezeshaji wa upatikanaji wa dawa muhimu kwa wote na matumizi sahihi ya dawa.

Hivyo basi ili kuwezesha upatikanaji wa dawa kwa watu serikali kwa kufuata miongozo ya Shirika la Afya Duniani (WHO), inasisitiza matumizi ya dawa asilia, kwani dawa ambazo zina hatimiliki ni za ghali sana hivyo matumizi ya dawa asilia huongeza uwezo wa kununua dawa nyingi zaidi na hivyo kuongeza upatikanaji kwa watu wengi zaidi.

Ili kuhakikisha kuwa dawa hizi asilia (generic) zinakidhi viwango vya ubora, Serikali ilianzisha Mamlaka ya Udhibiti wa Ubora wa Chakula, Dawa na Vipodozi (TFDA) ili kuhakikisha kuwa suala hili linasimamiwa vizuri na kitaalamu.

Kama tulivyoona hapo mwanzo kwamba jina asilia la dawa ndilo jina linalotambulika kote duniani, hivyo waganga na wafamasia wanafundishwa dawa kwa kutumia majina asilia na si majina ya kibiashara. Kutokana na miongozo hiyo na Sera ya Taifa ndio maana orodha ya dawa ya MTBA inatumia majina asilia na si vinginevyo.

Vilevile MTBA imesajili vituo vya kutolea tiba vile tu ambavyo vimesajiliwa na Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, ili kumhakikishia mfaidika wa Mfuko anapata huduma bora kwa gharama zinazokubalika, hii ikiwa ni pamoja na kupata dawa asilia zenye ubora.

Mfuko unaamini vituo hivi vinatunza dawa ambazo ubora, uwezo wa kutibu na usalama wake vimehakikiwa TFDA. Hata hivyo, pale ambapo dawa inayopatikana ni ile yenye hatimiliki pekee, basi Mfuko hulipia wanachama wake. Mfano Cellcept kwa wagonjwa waliobadilishiwa figo au ilivyokua kwa Coartem katika tiba ya malaria.

Kwa kumalizia ningependa kuwafahamisha mambo mawili muhimu. Kitaalam brand product ni ile dawa iliyotolewa na mtengenezaji wa kwanza yenye hatimiliki pekee. Watengenezaji wengine wanaofuata dawa hizo huitwa generic products hata kama imetengenezwa na viwanda vikubwa vya Ulaya na Marekani.

Ningependa mfahamu kwamba bei ya dawa inategemea na gharama za uzalishaji ndio maana dawa zilizotengenezwa Ulaya na Marekani ni ghali kuliko dawa zilizotengenezwa Asia na Afrika hii imepelekea watu wengi kufikiria kwamba dawa zote za Ulaya na Marekani ni brand product na zile za Asia na Afrika ndizo generic pekee, kumbe sivyo. Kama jambo hili lilikuwa linakutatiza natumaini umepata mwanga wa kutosha.


000000000

wapendwa ndugu zangu hasa wana blog napenda kuwafahamusha kuwa mimi noor shija mwandishi wa magazeti ya uhuru, mzalendo na burudani nimeamua kuingia kilingeni kushirikiana na nanyi katika kuhabarisha watu kupitia blog.

pia napenda kuwaletea tanzia ya mwandishi mwenzangu katika magazeti ya uhuru marehemu Ramadhan Kinyonya.

Imehaririwa: 24.09.2008 0101 EAT
Gazeti: Uhuru



Mwandishi Uhuru afariki dunia


KALALE SALAMA KINYONYA





Na Mwandishi WetuMWANDISHI wa habari wa Kampuni ya Uhuru Publications Ltd (UPL), inayochapisha magazeti ya Uhuru, Mzalendo na Burudani, Ramadhan Kinyonya amefariki dunia.Kinyonya (40), alifariki dunia jana saa 7.00 mchana katika Hospitali ya Taifa Muhimbili, Dar es Salaam alikokuwa amelazwa kwa matibabu tangu wiki iliyopita.Alifikishwa hospitali hapo kutokana na kusumbuliwa na ugonjwa wa homa ya mapafu.Kinyonya alijiunga na UPL mwaka jana. Aliwahi kufanya kazi katika magazeti ya Mtanzania, Majira, Mwananchi na Kampuni ya Global Publishers, inayochapisha magazeti ya Uwazi na Champion.Hadi mauti yalipomfika, Kinyonya alikuwa mwajiriwa wa UPL, akiwa mwandishi wa habari za michezo wa gazeti la Uhuru.Kwa waliomfahamu Kinyonya wakati wa uhai wake, alikuwa mchapakazi hodari, mcheshi na mtu wa utani, aliyependa kutaniana na wenzake katika mambo mbalimbali.Taratibu za mazishi zinaendelea kufanywa na ndugu wa marehemu. Taarifa zaidi kuhusu wapi na lini atazikwa zinatarajiwa kutolewa leo.Kinyonya alizaliwa mwaka 1968 mkoani Shinyanga. Alisoma katika shule za msingi na sekondari mkoani humo hadi mwaka 1987.Baadaye alijiunga na mafunzo ya cheti cha uandishi wa habari, elimu ya kompyuta na upigaji wa picha.